Information & Resources

Find information and resources to help manage your pain.

Get Help & Support

Find the tools you need to
help you manage your pain.

Get Involved

Help make a real difference to people
in the UK living with chronic pain.

About Us

Find out about Pain Concern and how
we can help you.

Nakala – Programu 71 ya Airing Pain: Protect our Girls

[Kwa habari zaidi kuhusu ukeketaji wa wanawake, tafadhali tazama waraka wetu wa habari za ukweli kuhusu ukeketaji wa wanawake.]

Maumivu endelevu na mapambano ya kukomesha ukeketaji wa wanawake.

Zaidi ya wanawake 100,000 nchini Uingereza wameathirika na ukeketaji wa wanawake pamoja na athari mbaya za muda mrefu ikiwemo maumivu endelevu. Janet Graves ameweza kusikia kutoka kwa waathirika wa ukeketaji wa wanawake na kwa wataalamu wa huduma ya afya wanaowatibu kuhusu desturi hii iliyoingizwa kitamaduni na namna ya kuing’oa.

Hana Gibremedhen na Valentine Nkoyo wanazungumzia athari ya kukeketwa walioipata wakiwa kama watoto juu ya afya yao ya kisaikolojia na ya kimwili na pia kuathiri uhusiano wao. Nkoyo pia anaelezea namna taasisi yake ya Mojato Foundation inavyohamasisha kupinga ukeketaji wa wanawake katika jamii zilizoathirika.

Uzoefu wa Gibremedhen wa maumivu ya kudumu yasiyotambuliwa baada ya ukeketaji wa wanawake unasisitizia ukosefu wa maarifa miongoni mwa wataalamu wa huduma ya afya. Kliniki zenye uzoefu wa kuona wanawake waliokeketwa ni muhimu sana, anasema Mkunga Mtaalamu Juliet Albert, kama wanatakiwa kupata huduma wanayoihitaji. Mkunga, ‘mpiganaji’ dhidi ya ukeketaji na mwasisi wa the Hope Clinic Aïssa Eden anatoa kisa chake na kusisitiza umuhimu wa elimu katika kuhakikisha usalama wa kizazi kijacho.

Valentine Nkoyo: wakati kisimi chote na midomo ya ndani na ya nje ya uke vimekatwa na kila kitu kimezibwa pamoja na likaachwa tundu dogo sana, unajua, kama kichwa cha njiti ya kiberiti. Na hiyo ni kwa ajili tu ya kuruhusu mkojo au damu ya hedhi kupita hapo. Unaweza kumfikiria mwanamke anaye fanya mapenzi na mwanamume katika tundu hilo dogo sana?

Hii ni Airing Pain, programu ambayo inaletwa kwenu na Pain Concern, shirika la msaada la Uingereza linalotoa taarifa na msaada kwa wale wanaoishi na maumivu miongoni mwetu na kwa wataalamu wa huduma ya afya.

Mimi ni Paul Evans na toleo hili linafadhiliwa na ruzuku kutoka Rosa, Mfuko wa Uingereza wa Wanawake na Wasichana.

Nkoyo: Siku ya harusi yao, huo ni wakati ambao mwanamme anatakiwa kufungua, wanapaswa kutumia nguvu kuingia tundu hilo dogo sana – unaweza kufikiria – na mara nyingine kama hawawezi kulifanya hilo, wanawake hulazimika kukatwa na mwanamme anapaswa kulala naye siku ya harusi. Hayo ni mateso. Kuzaa mtoto, mtoto anawezaje kutoka hapo? Hizi ni athari za kutisha wanawake wanaishi nazo.

Paul Evans: Ukeketaji wa wanawake unahusu taratibu zote ikiwemo uondoaji wa sehemu au kamili wa viungo vya nje vya uzazi vya mwanamke au jeraha jingine katika viungo vya uzazi vya mwanamke kwa sababu isiyokuwa ya kimatibabu. Nchini Uingereza inakadiriwa kwamba zaidi ya wanawake 100,000 wanaishi na athari za ukeketaji na wasichana elfu sitini wapo katika hatari.

Kwa toleo hili la Airing Pain Janet Graves atazungumza na waathirika, madaktari na wale wanaofanya kazi ili kukomesha desturi hii iliyoingizwa kitamaduni.

Juliet Albert: Jina langu ni Juliet Albert. Mimi ni mkunga mtaalamu wa ukeketaji wa wanawake. Ninafanya kazi katika Queen Charlotte Hospital, ambayo ni sehemu ya Imperial College Healthcare NHS Trust pia ni kiongozi wa mradi wa Acton African Well Woman Clinic.

Kuna aina nne tofauti za ukeketaji wa wanawake. Kwa jumla, ukeketaji wa wanawake huainishwa kama utaratibu wowote ambao una madhara na hauna kabisa faida za afya, ni hivyo utaratibu ambao unafanywa katika viungo vya uzazi vya mwanamke. Kuna aina nne tofauti za ukeketaji wa wanawake: aina ya 1 ni ambapo kifuniko cha kisimi au kisimi chenyewe kimeondolewa au kimekatwa; aina ya 2 ni ambapo kisimi na kifuniko cha kisimi na sehemu ya midomo na sehemu ya mbele vimeondolewa; aina ya 3 ni ambapo kisimi na kifuniko cha kisimi, wakati mwingine, na sehemu kubwa ya midomo vimeondolewa na kisha sehemu hiyo inashonwa kuunda kovu la mbele, na kuacha tundu dogo mno la kupitia mkojo na damu ya hedhi; na aina ya 4 ni taratibu nyingine yoyote, ambayo hujumuisha uchomaji wowote wa kitu kikali, utoboaji, uvutaji wa midomo, kimsingi, kitu kingine chochote ambacho kinafanywa katika viungo vya uzazi vya mwanamke.

Valentine Nkoyo: Jina langu ni Valentine Nkoyo na kwa asili ninatokea Kenya, katika jamii iitwayo Maasai. Nilikuwa na umri wa miaka 11 ambapo siku moja asubuhi mama yangu aliniita jikoni, alikuwa amemaliza kukamua ng’ombe maziwa na akasema ‘kuna kitu ambacho nataka kukizungumzia na wewe’. Na akaniambia, ‘umefika wakati wa wewe kuwa mwanamke’. Na sikujua hilo lilimaanisha nini. Na kisha nikamuuliza ‘unamaanisha nini, ninahitaji kuwa mwanamke? ’ Akasema ‘umefika wakati wa wewe kukeketwa. Wewe na dada yako mmekuwa wakubwa wa kutosha sasa’.

Hivyo jioni hiyo palikuwa na sherehe kubwa, chakula kingi na pombe na wanaume na wanawake walikuwa wanaimba na dada yangu na mimi na wasichana wengine wawili katika kijiji changu walikuwa wanaenda kukeketwa katika wakati huohuo. Na jioni, dada yangu na mimi tuliondolewa na tukanyolewa kwa sababu tunahitaji kuwa wasafi na tukapewa nguo mpya ambazo tulikuwa tunaenda kuzivaa wakati wa mchakato wote. Bibi zeu na shangazi zetu walitupa zawadi jioni hio na kisha tulitakiwa kupewa zawadi asubuhi na wajomba zetu baada ya kukeketwa.

Na kisha asubuhi majira ya saa kumi na mbili kamili tulivua nguo zetu na tukapewa blangeti ndogo, tunaziita lessos (kanga) na tukafunikwa nazo. Na tulikuwa na baridi sana, baridi kali mno. Dada yangu na mimi na wasichana wengine wawili kutoka kijijini hapo, tulipelekwa porini ambako walikuwa wanaenda kutekeleza upasuaji na walikuwa na kama kipande kikubwa cha kitambaa ambacho walikitandika ardhini na kisha palikuwa na ngozi ya mnyama juu.

Hivyo dada yangu alikuwa kushoto na wasichana wengine wawili kutoka kijijini hapo walikuwa kulia kwangu na wanawake wawili walishika miguu yangu na kuifungua, na kulikuwa na wanawake wengine ambao walinibana kwa nyuma, hivyo sikuweza kutikisika. Sikuweza kutikisa mikono yangu na sikuweza kutikisa miguu yangu na walikuwa wamekaza mno… kamwe sikuwahi kuhisi nimepanuliwa kama vile.

Ninakumbuka nilipotazama juu nikamwona mkeketaji na eeh – Mungu wangu – ninaweza kukumbuka kila kitu alichovaa. Ninaweza kukumbuka mapambo ya vito aliyovaa, rangi ya nguo zake… uso wake haujanitoka kamwe. Kila wakati ninapolizungumzia hili, bado uso wake upo. Si kitu ambacho kitatoeka, kwa sababu huyu ndiye mtu ambaye ataniadhibu katika maisha yangu, mtu ambaye ataniondoa kipande. Na ninakumbuka, nilifumba macho yangu kwa sababu sikutaka kumwona mpaka ulipofanywa upasuaji.

Hivyo nilifumba macho yangu. Na nilipofumba macho yangu niliweza kuhisi dada yangu akitikisika lakini hakuweza kupiga kelele yoyote na wanawake walikuwa wanasema ‘Usiwe mwoga! Usiwe mwoga!’ Na siwezi kukumbuka kiasi cha muda uliotumika lakini niliweza kuhisi anapambana nao lakini hakuweza kulia. Na kisha hilo likasimama na nikafumbua macho yangu na kisha nikamwona yule mwanamke tena na kisha nikayafumba tena, sikutaka kumwona tena. Kisha nikahisi mfinyo mkali sana kwenye kisimi changu na papo hapo nikaanza kuhisi wembe. Kwa kweli alitumia wembe ule ule alioutumia kwa dada yangu. Na nilianza kuhisi kila mkato aliokuwa anaufanya. Niliuhisi.

[Akitoa machozi] Na wanawake nyuma yangu walikuwa wanasema ‘Wewe ni msichana shujaa. Jikaze, tulia na hii itaisha hivi punde.’ Lakini nilihisi kama ni ya maisha yote. Na hasira ilikuwa… Sikuelewa kwa nini nilipaswa kufanyiwa ukeketaji. Ni kitu chenye kuumiza mno – hata huwezi kuyaelezea maumivu.

Na nakumbuka, walikuwa wanasema ‘Usilie!’ Lakini nilikuwa ninalia kwa ndani, lakini sikutaka kuiaibisha familia yangu kwa sababu ukipiga kelele au ukilia, hiyo inaweza kuwa ni doa daima. Na hata kwa mwanamme ambaye atakuoa, watajua kuwa ulilia ulipokuwa unakeketwa. Ni kitu fulani cha kisaikolojia ambacho huwezi kuishi nacho, hivyo unalia kwa ndani tu.

Kufanya mambo kuwa mabaya zaidi, alipomaliza kunikeketa, alichukua maji yenye chumvi na akamimina kwenye… kwenye kidonda kibichi. Na hiyo ilikuwa ni jahannamu. Siwezi hata kuelezea nilivyohisi, ilikuwa mbaya sana. fikiria kama una jeraha dogo mno na mtu aweke chumvi hapo, inatisha mno. Ni maumivu yale yale. Na nikifikiria kuwa mtoto mwengine anakaribia kufanyiwa hivyo, inanisikitisha sana, inanikasirisha sana.

Hivyo wakawakeketa wasichana wengine. Nilikuwa dhaifu mno, walinisaidia kusimama na kisha tukaenda na kusimama nje ya chumba tulichotakiwa kuponea. Wajomba zetu walitakiwa kutupa zawadi, hivyo tulizawadiwa ng’ombe, kondoo na, unajua, hela. Na ninakumbuka nilipotazama chini [analia kwa sauti] na nilikuwa nimesimama katika dimbwi la damu la damu yangu mwenyewe, niliweza kuiona ikimiminika. [Analia kwa sauti] sikuweza kufahamu kwa nini nilipaswa kupata maumivu yale, bado eti kulikuwa na watu wanasema kilikuwa ni kitu kizuri. Lakini hakikuwa kizuri na maumivu yalikuwa makali… si kitu unachoweza kukielezea.

Zawadi hazikuwa na maana kwangu, kwa sababu nilipokeketwa tu nilijua kitu kinachohusu maisha yangu kimeondolewa. Hivyo baada ya kupewa zawadi, tulirudishwa chumbani na nikapoteza fahamu. Ninakumbuka nilipopata fahamu tena walikuwa wanamimina koka-kola kooni kwangu. Hawakuweza kunipeleka hospitalini kwa sababu ingekuwa mbaya na wangeweza kukamatwa kwa kunikeketa. Lakini nilikuwa dhaifu sana kwa muda wa wiki tatu zote tulizotakiwa kupona.

Niliendelea kupata kumbukumbu za nyuma na kuona watu hawa ambao walikuwa wananifukuza, pengine ili kunikata koo langu au kuondoa kitu; na kisha nilijaribu kutoroka na walipokaribia kunikata niliamka. Kisha maumivu ni pale unapoamka haraka kwa sababu bado una kidonda na kisha kinaweza kikauma zaidi.

Tulipaswa kuchungwa kwa muda wa wiki tatu na kila siku walitumia maji yenye chumvi na Dettol, kipukusi, na harufu ya kipukusi, naichukia. Hata kama madaktari wameshauri hilo [kwa huzuni mno] siwezi kuitumia kwa sababu inanirudishia kumbukumbu. Ninafikiri athari za kisaikolojia zimeendelea kwangu. Si kitu ambacho kila mtu anatakiwa kukipitia.

Albert: Kwa bahati mbaya kuna matatizo mengi ya maumivu ya muda mrefu kama matokeo ya ukeketaji wa wanawake. Tunawaona wanawake katika kliniki yetu wenye maumivu ya muda mrefu, maumivu makali ya msamba kwa sababu ya ukeketaji, kwa mfano, maumivu ya kutoka mkojo, maumivu wakati wa kujamiiana, wakati mwingine maumivu ya kuendelea. Pia tunawaona wanawake ambao wanapata maumivu, tena wakati wa kujamiiana, kwa sababu, kwa mfano, kama wana aina ya 3 ambayo ni mbaya sana. Baadhi ya wanawake, maumivu yao ni kutokana na kuzaa watoto, ambayo ni matokeo ya kuzaa watoto na ukeketaji. Hivyo inatofautiana mno. Na kisha wanawake wengi wana maumivu mengi ya hisia. Hivyo tunaona wanawake, kwa mfano, ambao wanaweza kuwa na aina ya 1 ambayo labda si mbaya sana, lakini watakuwa na kumbukumbu zote za kukandamizwa, kutokwa damu, maumivu, bila kutumia ganzi. Na, matokeao yake, maumivu yao ya kisaikolojia ni makali mno, vibaya sana.

Hana Gibremedhen: Jina langu ni Hana. Ninatoka Afrika Mashariki, Ethiopia, lakini kwa asili ninatoka Eritirea. Nilipokeketwa nilikuwa nina umri wa miaka tisa takriban. Na ilikuwa asubuhi mapema nilipoambiwa niende chumbani, chumba kitupu na kisha mwanamke – si mkunga anayestahili lakini [mkunga] wa kitamaduni – aliniambia nikae humo. Na watu wengine wawili, walikuwa wameshika miguu yangu na kisha baada ya hapo ilikuwa inauma sana.

Kwa kawaida wanalifanya hili katika umri mdogo, [wakati ukiwa] msichana mdogo baada ya kuzaliwa – wiki 18 au zaidi kidogo, wakati huo ndiyo ambao wanakeketa kwa kawaida. Lakini kwa sababu fulani mimi nilichelewa, nilipokuwa nina miaka tisa, hivyo ninatakiwa kufanyiwa. Nchini kwetu wanaamini kukeketa ni kama kumlinda mwanamke – kutoenda na wanaume mbalimbali, kukulinda, kukutuliza, lakini hawatambui kuwa baada ya kukeketwa kuna athari gani – inauma sana.

Baada ya kumaliza, inauma zaidi kwa sababu wanakuhudumia kwa vitu vya kitamaduni, kwa sababu huendi hospitalini wala hutibiwi kwa vitu vinavyostahili. Wanatumia mitishamba na kisha wanaiweka kwenye sehemu yako ya siri kila asubuhi. Inaunguza sana, inauma sana. siwezi kuisahau.

Albert: Mwanamke mwenye aina ya kwanza, ambaye labda amepata aina ya ukeketaji yenye kikomo kidogo cha mwili, anaweza kuwa na athari mbaya sana za kisaikolojia, ambazo zinaweza hata zisijitokeze mpaka anapokuwa mjamzito. Hivyo kuna wanawake ambao tumekutana nao ambao wamezika ukeketwaji wao na hawajaufikiria, hawajauzungumzia na ghafla, wakati wa mimba na wa kuzaa mtoto, ghafla wanapata kumbukumbu za nyuma na tukio lote linawarejea tena, kwa sababu unaweza kufikiria kwa dhahiri wakati wa uchunguzi wa uke, ghafla inakumbusha sehemu walipokuwa alipokuwa mtoto wakati ukeketwaji wao ulipotekelezwa.

Hivyo, haijalishi sana walipata aina gani, inaweza kuwa kwamba kuzaa mtoto kukawa na athari kali za kihisia. Na kisha bila shaka tuna wanawake ambao wana aina mbaya mno za kimwili, kama aina ya 3 hasa, ambapo labda wameweza hata kupambana ili kuwa wajawazito, kwa sababu kama wana tundu dogo sana – kama ni mduara upatao nusu sentimita – upenyaji wakati wa kujamiiana unakuwa ni wenye maumivu makali kama si wenye kushindikana. Tuna wanawake watatu au wanne kila mwaka ambao wanakuja kliniki kwetu ambao ni wajawazito, licha ya kuwa na tundu dogo mno kama hilo. Na siku zote ninasema, ‘usiwe mjinga na kufikiri haiwezekani kwa sababu inaweza ikawezekana’.

Gibremedhen: Tangu niwe mjamzito, nilikuwa na maumivu muda mwingi. Na wakati mwingi wa kuzaa, ilikuwa ni jinamizi kwangu. Ilikuwa ni siku nne za usiku na mchana ili niweze kuzaa, kwa sababu daktari ambaye alinichunguza alisema nitashonwa kwa sababu ya kukeketwa kwangu. Si rahisi kufunguka inavyostahili na kisha kuzaa kawaida.

Albert: Kwa wale wanawake wenye aina mbaya sana ya 3, wanahitaji kufunguliwa, inapendeza kabla ya kuzaa – kabla ya kwenda leba – kwa sababu kwa kweli kufanya uchunguzi wa uke kuna maumivu sana, pia ngumu sana kwa mtu anayejaribu kulifanya hilo. kuingiza katheta ya mkojo ni ngumu sana na kama mwanamke anafika leba, kwa mfano. Baadaye sana labda anapokuwa tayari yuko katika hatua ya pili, tayari anasukuma, kisha inaweza kuwa taratibu ya dharura kumfungua kwa mtu ambaye labda kamwe hata hajaona mwanamke aliyekeketwa kabla na labda hajui nini wanafanya. Inaweza kumaanisha kuwa mwanamke ataishia kuzaa kwa kupasuliwa kwa sababu mkunga hajui njia bora ya kulishughulikia.

Kisha baada ya kuzaa pia kuna matatizo mengi, pamoja na mpasuko mbaya sana kwa sababu wana tishu nyingi zenye kovu katika eneo hilo. Kwa kiasi kikubwa wanaonekana kupata hemoraji baada ya kujifungua, kutokwa damu nyingi na kisha kwa sababu hiyo, kwa dhahiri, maumivu makali ya mwili.

Gibremedhen: Nesi, hawana elimu yoyote ya ukeketaji. Na nilipozaa mtoto wangu, baada ya mwezi… kwa kweli nilipata miezi minne ya maumivu na nilipoenda hospitalini na kuwaambia ‘bado nina maumivu. Ninaposimama ninahisi kuwa kitu kinanikandamizia chini.’ Ilikuwa kama nilikuwa ninatikisika katika mwili wangu. Na nilipokwenda kwa daktari wangu muda wote, walisema mishono yote ni mikavu na huna tatizo lolote, lakini hawagundui nini kinaendelea ndani.

Albert: Wakati mwingine wakati wanawake wanaenda hospitalini, ninafikiri – au labda hata kwa daktari – na wakachunguzwa, kwa mara ya kwanza katika viungo vya uzazi, inaweza kuwa mtu hajawahi kuona ukeketaji kabla. Mnasikia hadithi kutoka kwa wanawake na pia kuna utafiti, kwa kweli – Forward alifanya utafiti uitwao ‘The Peer report’, ambapo wanawake walieleza mshtuko wa wataalamu wa huduma ya afya walipowaona, ukeketwaji wao na kuwaleta wataalamu wengine wa afya ili watazame. Wakati mwingine hata walishtuka kwa sauti kwa namna walivyoshtushwa na kwa kukata tamaa huwafadhaisha sana wanawake wenyewe.

Hivyo ninafikiri ni muhimu sana kuwa na wataalamu wa ukeketaji wa wanawake ambao mwanamke anaweza kuhamishiwa pia. Ili, kwa mfano, kama mwanamke ataenda kwenye kipimo cha uzazi, kama nesi huyo au daktari hajaona ukeketaji kabla na amefahamu kuwa haionekani sawa kama ionekanavyo kwa kawaida – sipendi kutumia neno ‘kawaida’ kwa sababu najua linaweza kuwafadhaisha wanawake – wanaweza kuwahamishia kwa mtaalamu wa ukeketaji. Na mjni London, kuna kliniki kadhaa za wataalamu wa ukeketaji, lakini nyingi ni hospitali zinazohusu au zimeunganishwa na huduma za uzazi na kliniki, hivyo ni nadra sana kupata kliniki ya jamii kama yetu, ambayo iko wazi kwa wanawake wasiokuwa wajawazito pia.

Kuna kliniki Bristol ambayo ilifunguliwa mwaka jana ambayo inaongozwa na daktari, ambayo inafuata mtindo wetu katika Acton, lakini hakuna huduma nyingi zinazofanana na hizi. Na, ijapo kuwa London ina kliniki nyingine, kama nilivyosema, ambapo wanawake wanaweza kufika… kuna kliniki ya ukeketaji maarufu sana Birmingham, moja mjini Oxford… Hivyo kuna vituo vya ubora, lakini pia kuna sehemu ambapo kwa kweli hakuna kitu kwa wanawake. Kwa hivyo kuna vituo vyenye ubora, lakini pia kuna sehemu ambazo hakuna chochote anachoweza kupata mwanamke. Huenda kukawepo na vikundi vya kijamii au mashirika ya sekta ya tatu lakini hawana njia ya kufikia huduma za NHS za mtaalamu. Na hili ni tatizo kwa mwanamke anayeishi mjini Newcastle kuweza kukutana na mimi mjini London kidhahiri ni vigumu sana.

Tulikuwa na mwanamke anayetoka Ireland Kaskazini miezi miwili iliyopita. Alisema aliondoka nyumbani saa kumi kamili asubuhi ili kusafiri (kwa ndege) kuelekea London kuja katika kliniki yetu kwa sababu hakujua pakwenda na alikuwa amezaa watoto watatu kwa upasuaji. Wawili miongoni mwao walizaliwa mjini Newcastle na mmoja Ireland Kaskazini na alisema wakati wa kuzaa kwake kwa upasuaji hakuna mtu yeyote alitaja ukeketwaji wake hata mara moja. Sasa ni watu wapatao watatu ambao wameweka katheta ya mkojo na hawajataja alikuwa na aina mbaya ya 3 ya ukeketaji. Hivyo kuna matatizo ya waziwazi kwa wataalamu wa huduma ya afya ya kutojua namna ya kuwasaidia wanawake wenye ukeketaji.

Aïssa Eden: Jina langu ni Aïssa Eden. Mimi ni mkunga lakini pia ni mkunga mtaalamu katika masuala ya ukeketaji na mimi pia ni wale tunaowaita ‘mwathirika wa ukeketaji’, lakini ninapenda kujiita ‘mpiganaji’.

Ukiangalia usuli wa desturi ya ukeketaji wa wanawake, inafanywa na wanafamilia, bibi au mama – mtu unayemwamini, ambaye atakupeleka sehemu, ambapo utapata maumivu makali mno katika maisha yako, hali mbaya mno katika maisha yako. Hivyo, kuamini masuala inaweza kuwa moja ya athari za kisaikolojia za ukeketaji.

Ilifanywa nilipokuwa nina umri wa miaka sita pamoja na dada yangu mdogo, alikuwa ana umri wa mwaka mmoja tu. Na nililia kwa hatia kwa sababu, kwangu mimi, dada yangu hakupaswa kufanyiwa vile. Ilitekelezwa kwetu sisi wawili kwa sababu nilikuwa katika mchakato wa kusafiri kuelekea Ufaransa. Hivyo alikuwa hajapangiwa katika muda huu – walifanya hivyo kwa sababu mimi ndiyo nilikuwa ninasafiri. Walifikiria, ‘oh, acha tuwafanyie wote wawili’. Hivyo nilikuwa na hatia kwa muda mrefu kwa ajili ya dada yangu kwa sababu nilifikiri lilikuwa ni kosa langu.

Nilianzisha kliniki – niliita the Hope Clinic – ili kutoa huduma ya jumla kwa wanawake na familia zao. Tunafanya kazi na wanawake na tuna mradi, tuna mpango hasa kwa mwanamke huyu, kama huduma binafsi sana. Lakini pia ni elimu na kinga kwa sababu wakati unapaswa kwenda kwa ajili ya afya, ninafikiri unakuwa umechelewa sana. Hivyo elimu na kinga ni muhimu sana. Hatutaki mtu yeyote afanyiwe ukeketaji.

Albert: Kwa wanawake ambao wamekuwa na aina ya 3 ya ukeketaji – aina mbaya mno – kuna utaratibu unaitwa kuondoa mshono au ‘kufungua’ kweli. Kwa kweli tunapasua kovu la mbele, ili tufunue tundu la uke na tundu la mkojo chini ya tishu za kovu. Na kisha tunashona mipaka ya tundu hilo ili kuzuia kuungana tena pamoja. Wakati mwingine kihistoria, hii ilikuwa inaitwa ‘urudishaji nyuma’ lakini tunajaribu kutotumia istilahi hiyo kwa sababu huwezi kurudisha ambacho kimeondolewa. Hivyo kwa wanawake wenye aina ya 3, kwa kweli kuna utaratibu wa kimwili ambao unaweza kufanyika wakati mwingine. Wakati mwingine haiwezekani kufanyaka, hivyo kwa wanawake endapo kuna utata zaidi, kwa mfano, ambapo wana uvimbe pia aina yao ya 3, au wakati mwingine ambapo tishu za kovu zimeungana na tundu la mkojo, inafanya uondoaji wa mshono kuwa mgumu sana. Hivyo kwa baadhi ya wanawake hatuwezi, lakini utaratibu huu wa kuondoa mshono wa tundu ni utaratibu mdogo sana kwa kweli na unaweza kufanywa chini ya ganzi ya mtaa katika hospitali isiyolaza.

Hivi karibuni tulikuwa na mwanamke ambaye alikuwa amezibwa kwa miaka karibu 40 na kwa kweli alichunguza kwa furaha kwamba mwisho wake alifunguliwa [anacheka]. Wanawake wengine ambao wamekuwa wana watoto kadhaa, ambao wamekuwa tunavyoita ‘kuondolewa mshono’, au wamezibwa, kati ya watoto na kisha, tena, ambao wamekuja kutuona kwa sababu wanataka kufungua.

Kwa wale wanawake ambao wamekuwa na aina nyingine ya ukeketaji, kwa kweli hakuna utaratibu wa kimwili tunaoweza kufanya. Kwa kweli, wanahitaji ushauri mwingi na msaada wa kisaikolojia. Hivi karibuni tulikuwa na mwanamke – mwanamke kijana – ambaye alikuja kutuona, ambaye alitaka kujua alikuwa ana aina gani. Nilipochunguza, nilimweleza kuwa alikuwa aina ya 1 na nikamweleza kuwa hatungeweza kurudisha chochote ambacho kimeondolewa – baadhi ya kifuniko cha kisimi chake kilikuwa kimeondolewa na kisimi chake kilikuwa kimeondolewa. Na alikuwa amefadhaika vibaya sana. Akasema ‘nataka unifanye niwe kawaida tena kama kila mtu mwengine, nataka urudishe walichoondoa.’ Na alikuwa amechanganyikiwa sana kwa sababu alikuwa anataka kitu ambacho hatukuweza kumpa.

Nkoyo: Niliahidi kuwa sitathubutu kukaa na kuangalia wapwa zangu wanaenda kufanyiwa nilichofanyiwa. Hivyo nilianza kuzungumza na wanafamilia mbalimbali na, mwaka jana tu, mama yangu, dada zangu na kaka waliahidi. Na ilinichukuwa muda mrefu, kuchukuwa simu na kuomba msamaha na nikisema ‘nitazungumzia kitu ambacho kwa kawaida hatukizungumzii kwa uwazi’. Na nilizungumza – huyu alikuwa kaka yangu kwa kweli – kwa sababu nilisema nilitaka ajue nilichofanyiwa na ninachoishi nacho. Na nikasema ‘ninataka uniambie kama unataka binti yako afanyiwe hivyo’. Na nilipoeleza kila kitu, alisema ‘kamwe sitaruhusu hilo litokee. Na nikijua kuhusu yeyote ambaye ana nia ya kufanya hivyo, nitachukua hatua.’

Hivyo kwa mimi, nimefanikiwa kushughulikia sehemu ya kisaikolojia ya suala hilo kwa kusaidia wengine. Hivyo Taasisi ya Mojatu ni taasisi isiyolenga faida. Tupo Nottingham na kwa kiasi kikubwa tunafanya kazi na jamii za Kiafrika na za Kikaribiani. Tunazalisha matoleo sita ya gazeti letu la jamii linaloitwa Mojatu na tunalitumia ili kukuza ufahamu wa masuala ambayo yanaathiri jamii za Kiafrika na za Kikaribiani.

Kitu muhimu sana kwa kweli ni kuwasaidia watu kufahamu sehemu ulipo msaada. Hivyo ambacho nimekuwa nikikifanya mimi mwenyewe ni kutoka na kuzungumza na waathirika na kuwapa moyo wanawake ambao wamefanyiwa ukeketaji watafute msaada wa kimatibabu. Na hilo halitasaidia hali zao za afya tu lakini pia litasaidia ukusanyaji wa data, kufahamu ukubwa wa tatizo kimtaa na pia kitaifa, ili hili lifanikiwe kwa njia bora zaidi. Lakini tunahitaji kupata juhudi zilizoratibiwa kutoka polisi, kutoka halmashauri ya jiji, kutoka katika jamii na pia kuhusisha waathirika.

Na sasa tuna kikundi cha Nottingham cha kuongoza ukeketaji wa wanawake. Na mimi ni sehemu ya bodi hiyo kama mwakilishi wa jamii. Na nafikiri hili lina nguvu sana, kuwaleta watu wote pamoja na kupata maoni ya kila mtu. Na, kwangu mimi, kitu ambacho nimekuwa nikijaribu kukifanya ni kuwatia msukumo waathirika wajue kuwa kwa kweli ni sawa kuzungumzia kilichowatokea na ni sawa kuwashirikisha watu wengine, kwa sababu hiyo ndiyo njia pekee watu wanaweza kuungana kwa kile kilichotokea na pia kuchukua hatua ili kusaidia wasichana. Na, kwa sehemu kubwa ya wafanyakazi ambao nimekuwa nikifanya nao kazi, wanasema imewatia nguvu sana kuhisi kuwa wao ni sehemu ya mchakato huu wa kufanya maamuzi kuhusu namna gani ukeketaji unaweza ukashughulikiwa. Na kwangu mimi, ninaamini kabisa kuwa wao ni kikosi chenye nguvu katika kujisaidia wenyewe kushughulikia maumivu ya kilichotokea na athari zote na kuwalinda wasichana wetu.

Evans: Huyo alikuwa ni mwathirika wa ukeketaji, Valentine Nkoyo. Kwa habari zaidi kuhusu Taasisi ya Mojatu nenda katika tovuti yake valentinenkoyo.com. na ‘Nkoyo’ inaandikwa ‘N’ ‘K’ ‘O’ ‘Y’ ‘O’. Taasisi nyingine zilizotajwa ni The Hope Clinic na tovuti yao ni fgmhopeclinic.co.uk na kuna orodha kubwa ya kliniki za ukeketaji na njia katika tovuti forwarduk.org.uk. Viungo vyote hivi vipo katika tovuti ya Pain Concern ambako unaweza kupakua hii na kila toleo la Airing Pain na pia nakala na habari zaidi kuhusu ukeketaji na mada nyingine zinazohusu maumivu. Unaweza kusoma kuhusu ukeketaji katika toleo la 62 la mwezi huu la gazeti la Pain Matters na, kama ninavyosema, maelezo yote haya yanapatikana katika tovuti ya Pain Concern painconcern.org.uk.

Nitakukumbusha kwamba wakati katika Pain Concern tunaamini kwamba habari na maoni yaliyopo Airing Pain ni sahihi na thabiti, zinazohusu hukumu bora iliyopo, siku zote unatakiwa kupata ushauri wa mtaalamu wako wa afya kuhusu suala lolote linalohusu afya yako na ustawi. Yeye ndiye mtu pekee anayekujua wewe na hali zako na kwa sababu hiyo hatua inayostahili kuchukuliwa kwa niaba yako.

Albert: Ninajisikia vizuri sana, kwa kweli, kwamba wanawake wengi tunaowaona katika kliniki zetu na hasa wanawake ambao wamepata maumivu katika kipindi cha miaka, bila shaka hawana nia ya kuwafanyia mabinti zao wenyewe na, kwa kweli, wanajisikia vizuri sana kuhusu kutowafanyia mabinti zao na wanafamilia wengine. Ninafikiri kuwa wanawake wanaelimika kuhusu utata wa afya wa ukeketaji na kwa kweli sasa wanaelewa kiungo kati ya vitu hivyo viwili.

Ninafikiri, kihistoria, unaweza ukafikiria ikiwa mwanamke hakuwa na elimu kuhusu anatomia yake, hakujua chochote kuhusu biolojia na mtu mwengine yeyote kuwa ni sawa nayeye, wasingefanya hata muunganisho kati ya ukeketaji na maumivu ya kimwili aliyonayo. Na sasa ninafikiri kuwa wanawake ambao wanaelimishwa katika nchi hii na wanawaona watoto wao wanaenda kupitia utaratibu wa elimu… Ninafikiri inapaswa kufanya usawa na matarajio makubwa kwa kweli ni dhidi ya desturi na wanaume pia – kwa kweli tunaona familia ambazo zinaelewa kuwa ukeketaji ni kitu kibaya.

Sasa, bila shaka, sipaswi kuwa mjinga kwa sababu nina uhakika kuna sehemu ndogo ambako kuna watu ambao bado wanataka kuendelea na desturi hii. Na wasiwasi wangu ni kwamba wakati mwingine wanaweza kufanya aina mbaya kidogo ya ukeketaji, kwa sababu wanaamini hii ni mila ya kitamaduni ambayo tunahitaji kuiendeleza na tukifanya aina mbaya kidogo, hiyo ni sawa. Hivyo tunatumia muda mwingi pia kuwaeleza wanawake kuwa hata aina mbaya kidogo sana, itakuwa na athari mbaya sana ya kisaikolojia na kwamba wanaelewa hilo ni ukiukaji wa haki za binadamu.

Nkoyo: Nina matumaini sana kuwa kwa kweli tunaweza kukomesha ukeketaji katika kizazi. Nilikuwa msichana wa mwisho katika familia yangu na nikatoa kipaumbele kwamba sitavumilia na kuona mtu yeyote katika familia yangu anaenda kufanyiwa hivyo, hivyo wanne katika wapwa zangu waliokolewa mwaka jana kufanyiwa ukeketaji. Kazi kubwa bado inahitajika na najua kuna watu safi sana huko, mtu kama Lynn Featherstone [mbunge wa zamani wa Liberal Democrat] amekuwa ni mwenye msaada sana katika kampeni na madaktari… kuna Dokta Comfort Momoh, kuna Forward, kuna Taasisi ya Mojatu… kazi zote tunazozifanya ili kuongeza utambuzi… haitatokea kesho, ni mchakato wa polepole, lakini tutaweza kushughulikia ukeketaji na ni wajibu wa kila mtu kuwachunga wasichana wetu.


Wachangiaji:

  • Juliet Albert, Mkunga Mtaalamu wa Ukeketaji wa Wanawake, Queen
  • Charlotte Hospital, Imperial College Healthcare NHS Trust na Kiongozi wa
  • Mradi katika Acton African Well Woman
  • Valentine Nkoyo, Taasisi ya Mojatu, Nottingham
  • Hana Gibremedhen, Taasisi ya Mojatu, Nottingham
  • Aïssa Eden, Mkunga Mtaalamu.
No votes yet.
Please wait...

Related resources

Comments

Comments are closed.

https://painconcern.org.uk/cordless-car-vacuum-cleaner-eraclean-best-handheld-vacuum/
https://painconcern.org.uk/cordless-car-vacuum-cleaner-eraclean-best-handheld-vacuum/ https://painconcern.org.uk/sex-toys-in-india-best-adult-products-online-sex-toys-store-for-men-woman/